Mchezaji nyota mstaafu wa mpira wa kikapu amefariki kwenye ajali ya helikopta huko Calabasas, California.
Bryant alikuwa akisafiri na watu wengine nane kwenye helikopta binafsi wakati ilipodondoka, kwa mujibu wa vyombo vya habari nchini Marekani.

Binti wa Bryant mwenye umri wa miaka 13 Gianna pia amefariki kwenye ajali hiyo, kwa mujibu wa TMZ. Ilisemekana walikuwa njiani kuelekea kwenye mazoezi ya mpira wa kikapu kitongoji cha Thousand Oaks.
Polisi mjini Los Angeles walithibitisha kupata miili ya watu nane eneo la tukio, lakini walikataa kuwataja waliokuwemo kwenye ndege hiyo.

Bryant umri miaka 41, alifahamika kwa kusafiri kwa helikopta katika michezo wakati akiwa nyota wa timu ya Los Angeles Lakers ambapo alikuwa akitumia helikopta aina ya Sikorsky S-76.
Shirika la masuala ya anga la Marekani limetaja helikopta iliyohusika katika ajali hiyo kuwa ni Sikorsky S-76, katika taarifa hiyo walisema shirika hilo (FAA) na Bodi ya Usalama wa Usafiri Kitaifa watachunguza ajali hiyo.
Polisi walisema helikopta ilidondoka kwenye eneo lenye muinuko mkali na vikosi vya huduma za dharura bado viko eneo la tukio.
Bryant na mkewe, Vanessa, walikuwa na watoto wa kike wanne: Gianna, Natalia, Bianca na Capri, ambaye alizaliwa mwezi wa sita mwaka 2019.

